Ripoti: Uchaguzi wa serikali za mitaa hautofanyika mwaka huu DRC
Uchaguzi wa serikali za mitaa ambao awali ulipangwa kufanyika mwaka wa 2019, hautarajiwi pia kufanyika mwaka huu. Nchi haiko tayari kuandaa uchaguzi huo, kulingana na ripoti ya Tume ya Uchaguzi, CENI, ambayo pamoja na mambo mengine inasimulia matatizo makubwa ya ukosefu wa fedha na vifaa.
Imechapishwa:
Katika ripoti yake Tume Huru ya taifa ya uchaguzi (CENI) imebaini kwamba ni vigumu kuandaa uchaguzi wa madiwani wa manispaa na madiwani wa sekta na wakuu wa maeneo mbalimbali, katika mazingira ya sasa. Sababu ya kwanza iliyotajwa katika ripoti hiyo ni ukosefu wa vifaa.
Katika ripoti hiyo wametaja ujenzi wa ofisi watakazotumia madiwani 11,000. Taasisi hizi ni aina ya wabunge katika ngazi ya chini katika maeneo yao, bila kusahau fedha za matumizi ya ofisi na mishahara ya maafisa hao.
Katika ripoti yake iliyowasilishwa bungeni, CENI imependekeza kwamba idadi ya halamashauri za manispaa ipunguzwe.
Kwa upande wake, Waziri wa Mawasiliano na Vyombo vya Habari, David-Jolino Diwampovesa Makelele, amebaini kwamba hakuna uamuzi wowote unaoweza kuchukuliwa kabla ya kupata matokeo ya mageuzi ya uchaguzi.
Waziri huyo Amekumbusha nia ya Félix Tshisekedi ya kuandaa uchaguzi huo wakati wa muhula wake wa miaka mitano.
Kwa upande wake, Ceni imependekeza, kwamba uchaguzi huo ufanyike mwishoni mwa muhula wa rais.