Maafisa wa afya wasitisha vita dhidi ya Ebola mkoani Ituri nchini DRC
Maafisa wa afya wanaopambana na maambukizi ya Ebola katika mkoa wa Ituri, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wamesitisha shughuli zao katika eneo la Biakato, kwa kuhofia usalama wao.
Imechapishwa:
Hatua hii imekuja, baada ya watu wengine saba kupoteza maisha katika eneo hilo, baada ya kushambuliwa na watu wenye silaha.
Pamoja na mauaji hayo, shirika la kiraia la CEPADHO limesema kuwa watu hao wenye silaha, wanaoaminiwa kutoka kundi la Mai Mai, walivamia maafisa wa polisi usiku wa Jumamosi.
Wiki hii pekee, imeripotiwa kuwa watu zaidi ya 60 wamepoteza maisha, baada ya kushambuliwa na makundi ya waasi, wakiwemo wale wa ADF Nalu.
Watalaam wa afya wameonya kuwa, ukosefu wa usalama hasa katika Wilaya ya Beni, umeendelea kusababisha mazingira magumu ya kudhibiti maambukizi ya Ebola ambayo kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa yamesababisha vifo vya zaidi ya watu elfu mbili.