Emmerson Mnangagwa arejea Zimbabwe
Aliyekuwa Makamu wa rais wa zamani wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa amerejea nyumbani jioni hii jijini Harare, kuongoza nchi hiyo baada ya kujiuzulu kwa Robert Mugabe siku ya Jumanne.
Imechapishwa:
Mnangagwa amepokelewa na maelfu ya watu waliofurika katika uwanja wa ndege kumkaribisha.
Shirika la Utangazaji nchini humo ZBC, limesema kuwa Mnangagwa aliyefutwa kazi na Mugabe na kukimbilia nchini Afrika Kusini, ataapishwa siku ya Ijumaa.
Wananchi wa Zimbabwe wameendelea kusherehekea kujiuzulu kwa Mugabe, huku wengi wakisema ni mwamko mpya wa kisiasa na kiuchumi kwa nchi yao.
Emmerson Mnagangwa, anatarajiwa kuongoza kwa muda kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka ujao.
Robert Mugabe alijiuzulu siku ya Jumanne Novemba 21, baada ya kushinikizwa kufanya hivyo.
Jeshi nchini humo lilianzisha mchakato wa kukosa imani na uongozi wa Mugabe baada ya mkewe Grace, kuonekana kuingilia uongozi wake.
Emmerson Mnangagwa alifutwa kazi wiki tatu zilizopita na kutoroka nchi hiyo kufuatia vitisho vya kuuawa.