Grace Mugabe arejea nyumbani licha ya kushtumiwa kumpiga mwanamke Afrika Kusini
Grace Mugabe, mke wa rais wa Zimbabwe Robert Mugabe amerejea nyumbani akitokea nchini Afrika Kusini baada ya kutofika Mahakamani siku ya Jumanne alikokuwa ameshtumiwa kwa kumpiga na kumjeruhi mwanamke mmoja.
Imechapishwa:
Bi. Mugabe amerejea nyumbani wakati, kukiwa na maswali mengi kuhusu ni kwanini hakufika Mahakamani, hata baada ya kuahidi kufanya hivyo.
Mwanamke mwenye umri wa miaka 20, amemtuhumu Bi. Mugabe kwa kumpiga kichwani na kumjeruhi akitumia kifaa cha umeme Jumapili iliyopita katika hoteli moja jijini Johannersburg.
Licha ya kuwepo kwa ripoti kuwa angekwenda Mahakamani, mke huyo wa rais Mugabe hajagusia madai dhidi yake.
Hata hivyo, Waziri wa maswala ya Polisi Fikile Mbalula, alishutumu kitendo hicho na kusema ni lazima afunguliwe mashtaka lakini haijafahamika ni vipi hilo halijafanyika.
Serikali ya Zimbabwe imethibitisha kurejea salama jijini Harare kwa Bi. Mugabe.