Ethiopia: Hatutaki wachunguzi wa kigeni
Ethiopia imekataa pendekezo la Umoja wa mataifa na Umoja wa Ulaya wa kutaka wachunguzi wa kimataifa kuingia nchini humo na kuchunguza vifo vya mamia ya watu wanaodaiwa kuuwawa kufuatia miezi kadhaa ya maandamano ya kuipinga serikali.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Waziri Mkuu Hailemariam Desalegn amewaambia waandishi wa habari mjini Addis Ababa kuwa tume ya kitaifa ya haki za Kibinadamu tayari inachunguza visa hivyo.
Bw Desalegn amesema ni lazima haki ipatikane kwa sababu kuna nia ya kushughulikia hilo ndani ya Serikali. Amesema uchunguzi umefanywa na matokeo yake yatawekwa wazi.
Hivi karibuni Bunge la Ethiopia liliongeza muda wa hali ya hatari iliyotangazwa mwezi Oktoba mwaka jana kwa miezi minne zaidi.
Mapema mwezi Aprili mjumbe maalum wa Umoja wa Ulaya kuhusu haki za kibinadamu aliitaka Ethiopia kushirikiana na Umoja wa mataifa kuhusu kuchunguza vifo vya mamia ya watu wanaodaiwa kuuwawa na vyombo vya dola.
Hata hivyo Waziri mkuu Hailemariam Desalegn ametetea hatua ya serikali yake kuongezea muda wa hali ya hatari iliyotangazwa mwezi Oktoba mwaka jana, akidai hali hiyo ilihitajika ili kuweza kukabiliana na baadhi ya watu ambao bado wana nia ya kuleta vurugu.