Waendesha mashtaka Cameroon wataka mwanahabari wa RFI ahukumiwe kifo
Viongozi wa Mashitaka katika Mahakama ya kijeshi nchini Cameroon wanapendekeza kuwa Mwanahabari wa RFI Hausa Ahmed Abba apewe adhabu ya kunyongwa kwa madai ya kushirikiana na kundi la kigaidi la Boko Haram.
Imechapishwa:
Abba amekuwa akizuiliwa tangu mwezi Julai mwaka 2015 baada ya kukamatwa akiwahoji washukiwa wa kundi la Boko Harama na kufunguliwa mashtaka ya ugaidi na kuwasaidia kutekeleza mashambulizi ya kigaidi nchini humo na nchi jirani.
Ombi hilo la viongozi wa Mashtaka limewashangaza watu wengi wakiwemo jamaa ndugu na marafiki wa Abba waliokuwa Mahakamani kusikiliza kesi hiyo siku ya Alhamisi.
Wakili wa Abba, Charles Tchoungang, amesema yeye hakushangazwa na ombi hilo kwa kile alichokisema kuwa, upande wa Mashtaka ulilenga kuipendeza Mahakama hiyo ya kijeshi.
Ushahidi uliotolewa dhidi ya Abba, haujaonesha kwa namna yoyote ile kuwa alikuwa anashirikiana na wanamgambo hao ambao wamesababisha mauaji makubwa hasa katika nchi jirani ya Nigeria.
Uongozi wa RFI umeendelea kulaani kuzuiliwa kwa Abba na kutaka kuachiliwa kwake huru mara moja bila ya masharti yoyote.
Majaji katika Mahakama hiyo ya kijeshi wanatarajiwa kutoa uamuzi wao tarehe 20 mwezi huu wa Aprili.