Raia wa Gambia wanasherehekea rasmi ushindi wa rais Adama Barrow
Rais wa Gambia Adama Barrow anasherehekea ushindi wake wa urais rasmi hivi leo jijini Banjul baada ya kushinda Uchaguzi Mkuu mwezi Desemba mwaka uliopita.
Imechapishwa:
Hafla hii inakwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 52 ya uhuru wa taifa hilo la Afrika Magharibi lilitawaliwa na Waingereza.
Marais mbalimbali hasa kutoka barani Afrika, na wawakilishi wengine kutoka Mataifa ya Magharibi watashuhudia sherehe hizo.
Awali, rais Barrow aliapishwa mwezi uliopita katika ubalozi wa nchi yake jijini Dakar nchini Senegal baada ya kiongozi wa zamani Yahya Jammeh kukataa kuondoka madarakani.
Rais Barrow ameahidi kuleta mabadiliko nchini humo na kurejesha hali ya kidemokrasia nchini humo ikiwa ni pamoja na kurejesha uhusiano wa Gambia na Jumuiya ya Kimataifa.
Tayari amesema kuwa Gambia imerejea katika Umoja wa nchi za Jumuiya ya Madola lakini pia kwa nchi yake kutoondoka katika Mahakama ya Kimataifa ya ICC.