Edgar Lungu aapishwa kuwa rais wa Zambia, ahimiza umoja wa Kitaifa
Rais wa Zambia Edgar Lungu ameapishwa kuongoza nchi hiyo kwa muda wa miaka mitano ijayo baada ya kutangazwa mshindi katika Uchaguzi Mkuu wa mwezi Agosti mwaka huu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Lungu ambaye aliingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka 2014 baada ya kufariki kwa rais Michael Satta, amewataka raia wa Zambia kuungana na kuwa kitu kimoja baada ya uchaguzi kukamilika.
“Uchaguzi sasa umekamilika, ni lazima tuungane pamoja na tuwe kitu kimoja,” aliwaambia maelfu ya raia wa Zambia.
Uchaguzi wa mwezi Agosti ulikuwa wenye ushindani mkali sana kati yake na mgombea wa upinzani Hakainde Hichilema aliyedai kuibiwa kura.
Kuelekea kuapishwa kwa rais Lungu, Hichilema alikwenda Mahakamani kupinga ushindi wake lakini Mahakama ya Kikatiba ikatupilia mbali kesi yake.
Hichilema ambaye amewania urais mara tano bila mafanikio, amesema sherehe za kumwapisha rais Lungu hazikuwa halali na zimekwenda kinyume na Katiba ya Zambia.
“Mahakama haikutoa uamuzi kuwa rais Lungu alishinda uchaguzi huu. Huu ni uvunjifu wa Katiba. Ukweli ni kwamba kura zetu ziliibiwa,” alisema Hichilema.
Viongozi kadhaa wa bara Afrika walihudhuria sherehe hizo zilizofanyaika jijini Lusaka akiwemo rais wa Zimbabwe Robert Mugabe.