Boko Haram yaendelea kutekeleza maovu
Nchini Nigeria kundi la kigaidi la Boko Haram limevamia miji miwili Kaskazini Mashariki mwa nchi hiyo na kuteketeza moto makaazi ya watu na kuiba vyakula.
Imechapishwa:
Walioshuhudia uvamizi huo wanasema wanamgambo hao waliwasili katika miji ya Galda na Fika katika jimbo la Yobe wakiwa ndani ya Malori na pikipiki na kuwafukuza wakaazi wa mji huo.
Rais Muhamadu Buhari aliyeapishwa Ijumaa iliyopita, aliahidi kulimaliza kundi hili ambalo limesabisha maafa ya maelfu ya watu na kuwateka raia wa Kaskazini mwa Nigeria kwa kipindi cha miaka sita iliyopita.
Wakati huo huo, baada ya kuapishwa juma lililopita, rais wa Nigeria Muhammadu Buhari anatazamiwa kujielekeza katika nchi jirani ya Niger, ambayo itakua ni ziara yake ya kwanza ya kikazi baada ya kuchukua hatamu ya uongozi wa nchi. baadaye atajielekeza nchini Chad.
Nchi hizi mbili Niger na Chad pamoja na Nigeria zinakabiliwa na mashambulizi ya Boko Haram. Hata hivyo rais Muhammadu Buhari ameapa kulitokomeza kundi la Boko Haram.
Rais Muhammadu Buhari anatazamiwa kuwasili katika mji mkuu wa Niger, Niamey Jumatano wiki hii, ambapo atakutana kwa mazungumzo na mwenzake wa Niger Mahamadou Issoufou.