Wahamiaji 300 wamekufa maji katika bahari ya Mediterranean
Wahamiaji 300 kutoka Afrika wamekufa maji katika bahari ya Mediterranean, baada ya boti mbili walizokuwemo kuzama maji, Jumatano Februari 1, huku tisa miongoni mwao wakiwa wamenusurika.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa mataifa linalowahudumia wakimbizi, UNHCR, watu zaidi ya 300 wanasadikiwa kuwa wamekufa maji, iwapo zitaongezwa ajali mbili zilizotokea hivi karibuni. Manusura wameingia katika kisiwa cha Italia cha Lampedusa.
Kwa mujibu wa mwandishi wa RFI, Roma, Anne Trecas, watu hao tisa walionusurika katika ajali hiyo ni kutoka nchi za Mali na Senegal, na wameokolewa na boti ya Italia. Manusura hao wamewasili mapema Jumatano asubuhi wiki hii katika kisiwa cha Lampeusa, huku wakielezea safari yao kwamba imekumbwa na hali ya sintofahamu, ambapo wao pekee ndio wamenusurika.
Boti hizo mbili ziliyokua zikiwabeba wahamiaji hao ziliondoka katika pwani ya Libya Jumamosi, mwishoni mwa juma lilopita. Kila boti ilikua ikibeba zaidi ya watu 100. Boti hizo zilikumbwa na dhoruba pamoja na mawimbi yenye mita 8 hadi 9.
Hayo yakijiri, takribani watu 203 walitoweka Jumatatu jioni wiki hii, baada ya boti mbili kupata ajali. Hata hivyo manuari ya jeshi la Italia ilijaribu kuokoa boti ya tatu iliyokua ikitokea Libya Jumamosi juma lilopita. Katika ajali hiyo watu 76 waliokolewa, lakini wengine 29 walifariki kutokana na baridi kali, licha ya kuokolewa.
Mpaka sasa shughuli za kutafuta miili ya watu waliofariki katika ajali hiyo zinaendelea katika bahari Mediterranean.