DRC: mapigano yatokea Beni, mashariki mwa Congo
Mapigano mapya yametokea jumatatu Novemba 3 katika kijiji cha Muzambaï wilayani Beni kati ya jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na kundi la waasi ambalo utambulisho wao haujajulikana bado.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa baadhi ya raia waliowasikia waasi hao wakizungumza, inasemekana kuwa kundi hilo lina watu ambao wamesikika wakizungumza kiswahili na kinyarwanda, jambo ambalo mkuu wa wilaya ya Beni, Bwanakawa Nyonyi amewataka raia wake wasipotoshwe nalo kabla ya uchunguzi kukamilika.
Mashirika ya Kiraia Mashariki mwa nchi hiyo yanasema, serikali ikishirikiana na wanajeshi wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani wanastahili kuongeza jitihada za kupambana na waasi wilayani Beni.
Mapiganao kati ya jeshi na kundi hilo la watu wenye silaha yameendelea katika kijiji hicho cha Muzambaï usiku wa Jumatatu kuamkia leo Jumanne Novemba 4.
Hakuna taarifa rasmi kuhusu hasara iliyotokea katika mapigano hayo, lakini mwanamke mmoja aliye tekwa nyara siku moja kabla inadaiwa kuwa ameachiwa huru, kulingana taarifa ziliyotolewa na mashirika ya kiraia.