Watu 10 wameripoitwa kupoteza maisha kwenye shambulio la bomu jijini Nairobi
Polisi nchini Kenya inawashikilia watuhumiwa wawili wa ugaidi baada ya mashambulizi mawili kutekelezwa kwenye soko moja jijini Nairobi nchini Kenya ,na kuua zaidi ya watu kumi na zaidi ya sabini kujeruhiwa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mashambulizi haya yanatekelezwa wakati huu mamia ya watalii raia wa Uingereza wakianza kuondolewa kwenye mji wa kitalii wa Mombasa baada ya nchi yao kutoa onyo kwa raia wake kutosafiri kwenye mji huo na kuwataka kuondoka.
Kitengo maalumu cha kupambana na ugaidi nchini Kenya NDOC kimesema kuwa shambulio la kwanza lilitekelezwa kwenye basi dogo la abiria huku lile la pili likitekelezwa kwenye soko la Gikomba ambapo watu wengi walikuwa kwenye shughuli zao za kawaida.
Msemaji wa hospitali ya taifa ya kenyatta amethibitisha hospitali yake kupokea miili ya watu 8 na wengine zaidi ya sabini ambao walikuwa wamejeruhiwa kwenye shambulio hili.
Shambulio hili linatekelezwa ikiwa umepita mwezi mmoja tu toka kutekelezwa kwa shambulio jingine kama hilo kwenye mabasi mawili jijini Nairobi na kule Mombasa ambapo watu zaidi ya kumi pia walipoteza maisha.
Mashambulizi haya yanadaiwa kutekelezwa na wapiganaji wa kundi la Al-Shabab lenye makazi yake nchini Somalia ambapo wapiganaji hao wameapa kutekeleza mashambulizi hayo hadi pale Kenya itakapoondoa majeshi yake.
Serikali ya Marekani imelaani mashambulio hayo na kuyaita ya woga kwa vile yamelenga raia wasiokuwa na hatia wala uwezo wa kupambana,na kuahidi kushirikiana na Kenya kukabiliana na ugaidi.