China na Urusi zakutana katika mkutano mkubwa wa kibiashara
Rais wa China Xi Jinping siku ya Ijumaa atakuwa mgeni wa heshima katika mkutano wa kiuchumi jijini Moscow, mkutano ambao unatoa picha halisi ya namna nchi hizo zimesimama pamoja kujenga uchumi wa mataifa yao.
Imechapishwa:
Rais Xi Jinping ambaye aliwasili nchini Urusi Jumatano ya wiki hii kwa ziara ya siku tatu, alimuelezea rais wa Urusi Vladimir Putin kama rafiki wa kweli kwa nchi yake.
Mkutano wa kiuchumi unaofanyika unalenga kutangaza fursa zilizopo za kibiashara kwenye mataifa yao pamoja na kutafuta nchi washirika zaidi wa kiuchumi tofauti na Marekani ambayo sasa inaonekana adui.
Akiwa nchini Urusi rais Xi Jinping ameshuhudia utiaji saini wa mikataba kadhaa ya ushirikiano ikiwemo mkataba wa kupanua wigo wa mtandao wa 5G wa kampuni ya Huawei ambayo imewekewa vikwazo nchini Marekani.
Katika hatua nyingine, rais Putin amesema hakusikitishwa na yeye kutopokea mualiko kuhudhuria maadhimisho ya miaka 75 tangu kumalizika kwa vita ya pili ya dunia.