Iraq: Marekani yaapa kuyaangamiza makundi ya kiislamu
Marekani imethibitisha kwamba itahakikisha imeyaangamiza makundi ya kiislamu, ambayo imeyataja kuwa ni maradhi yasiyotibika. Kauli hiyo ya Marekani inakuja baada ya makundi hayo kumnyonga mwanahabari wa Marekani, James Foley, na kutishia kumnyonga raia mwengine wa Marekani.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hayo yakijiri wapiganaji wa kikurdi wameanzisha ijumaa wiki hii mashambulizi dhidi ya wapiganaji wa kiislamu kwa lengo la kudhibiti maeneo yanayoshikiliwa na wapiganaji hao, viongozi wa kikurdi wamethibitisha.
Kwa mujibu wa Shirko Mirwanais, mmoja wa viongozi wa muungano wa vyama vya kikurdi (UP), mapigano hayo kati ya wapiganaji wa kikurdi na wale wa kiislamu wanaoshikilia baadhi ya maeneo nchini Iraq na Syria yamesababisha vifo vya watu wengi kutoka pande zote mbili.
“Wapiganaji wa kikurdi (Peshmerga) wameelekea katika mji wa Jalawla, huku wakiwatimua wapiganaji wa kislamu kwenye ngome zao”, amesema Mirwanais
Kiongozi mwengine wa muungano huo wa UPK, Mullah Bakhtia, amethibitisha kuanza kwa mashambulizi ya wapiganaji wa kikurdi dhidi ya wapiganaji wa kiislamu
Wapiganaji 10 wameuawa wakati walipokua wakijaribu kuuteka mji Jalawla uliyotekwa na waasi Agosti 11.
Jalawala ni mji uliyoko kilomita 130 kaskazini mwa mji mkuu wa Iraq, Baghdad na kwenye umbali wa kilomita zaidi ya 30 na mpaka wa Iran. Kwa sasa mapigano yanaripotiwa kando na mji huo.
Wakati huo huo watu wenye silaha wameshambulia waislamu kutoka dhehebu la Suni wakati wa swala ya Ijumaa katika msikiti kaskazini mashariki mwa Baghdad, na kusababisha vifo vya watu 32, viongozi wamethibitisha.
Hali hiyo imezua wasiwasi na lawama. Baadhi wamesema huenda watu hao wameshambuliwa na wanamgambo wa waislamu kutoka dhehebu la Shia, huku wengine wakibaini kwamba wapiganaji wa kiislamu wanaoshikilia baadhi ya maeneo ya Iraq, ambao ni kutoka dhehebu la Suni ndio wamehusika na shambulio hilo.