Urusi imeshambulia bandari ya Danube kwa mara ya nne tena.
Ndege zisizo na rubani za Urusi zimeshambulia wilaya inayozunguka bandari ya mto Danube ya Izmail nchini Ukraine kwa mara ya nne ndani ya siku tano, gavana wa eneo hilo amesema.
Imechapishwa:
Shambulio la hivi punde la usiku kucha, kwa kutumia ndege zisizo na rubani za Shahed zilizotengenezwa na Iran, lilichukua muda wa saa tatu, gavana wa eneo la Odesa Oleg Kiper amesema kwenye mtandao wa Telegram.
Hili ni shambulio la nne katika wilaya ya Izmail katika siku tano zilizopita," Kiper amesema.
Miundombinu ya kiraia na bandari, lifti na jengo la utawala viliharibiwa."
Dereva wa lori la kiraia alipata jeraha dogo la mguu, aliongeza.
Jeshi la wanahewa la Ukraine lilisema ndege 33 zisizo na rubani za Urusi zilirushwa usiku katika vikundi kadhaa, hasa katika mwelekeo wa wilaya za kusini za mkoa wa Odesa.
Mwezi uliopita shambulio sawa na hilo lilifanywa na likaharibu vibaya mabohari na maghala ya nafaka . Ukraine ina bandari mbili katika mto Danube, Reni na Izmail. Picha zinazoendelea kuonekana katika mitandao ya kijamii zinaonyesha jinsi Bandari ya Izmail ilivyoshambuliwa.
Izmail inapakana na Romania na imekua njia kuu ya usafirishaji wa bidhaa za Ukraine kufuatia Urusi kujiondoa katika mkataba wa nafaka uliosimamiwa na Umoja wa Mataifa mwezi Julai.
Haya yanajiri wakati huu marekani ikitangaza kuwa itasambaza makombora ya mizinga ya urani yaliyorutubishwa kwa Ukraine kama sehemu ya zaidi ya $1bn (£800m) katika msaada wa kijeshi na kibinadamu.
Urusi hata hivyo imelaani hatua ya kuipa Ukraine mizinga ya Marekani ya Abrams na silaha zenye utata zinazoingia hadi kwenye mavazi ya kujilinda dhidi ya silaha.
Tangazo hilo lilitolewa huku Ukraine ikiishutumu Urusi kwa kuwaua watu 17 katika shambulio la kombora eneo la sokoni.