Mjumbe wa Papa Francis kuzuru Ukraine kwa siku mbili
NAIROBI – Kadinali wa Italia Matteo Zuppi anaelekea mjini Kiev kama mjumbe wa kiongozi wa kanisa katoliki duniani Papa Francis kwa mazungumzo ya siku mbili na mamlaka ya Ukraine kuhusiana na vita vyake na Urusi.
Imechapishwa:
Zuppi, mkuu wa maaskofu nchini Italia, atazuru Kyiv kama mjumbe wa Papa matakatifu kati ya tarehe 5 na tarehe 6, ofisi ya Vatican imesema katika taarifa yake.
Kwa mujibu wa Vatican, ajenda kuu ya ziara hiyo ni kufanya mazungumzo ya kina na mamlaka nchini Ukraine kama njia moja ya kurejesha amani na utulivu.
Mwezi Mei mwaka huu, Vatican ilisema kuwa Papa Francis alikuwa amemuomba Zuppi kuongoza ujumbe wa amani kujaribu kupunguza wasiwasi katika mzozo unaoendelea nchini Ukraine.
Msemaji wa Vatican Matteo Bruni amesema hatua ya Papa kutuma ujumbe wake mjini Kyiv inaonyesha kwamba kiongozi huyo hajatupilia mbali juhudi zake za kutaka kuwepo kwa amani.
Papa aligusia kuhusu suala la kutuma ujumbe nchini Ukraine baada ya kurejea kutoka ziarani nchini Hungary mwezi April, japokuwa hakutoa maelezo Zaidi.
Zuppi, 67, aliteuliwa kuwa mkuu wa maaskofu nchini Italia akitokea katika jamii ya Wakatoliki wa Sant'Egidio ambao wamebobea katika masuala ya diplomasia na juhudi za upatikanaji wa amani.