Rais wa Paraguay afuta mpango wake wa kuwania muhula wa pili
Rais wa Paraguay, Horacio Cartes, alitangaza Jumatatu kuachana na mapendekezo yake tata yanayolenga kuwania muhula wa pili katika uchaguzi wa urais. Mpango huo wa rais Horacio Cartes ulisababisha maandamano na vurugu mwishoni mwa mwezi Machi.
Imechapishwa:
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumatatu, rais wa Paraguay alihakikisha kwamba amefuta nia yake ya kuwania muhula wa pili katika uchaguzi wa urais unaopangwa kufanyika mwezi Aprili 2018.
Mapema mwezi Machi Baraza la Seneti liliidhinisha mageuzi ya katiba ili kumpa nafasi rais Horacio Cartes kuwania muhula wa pili. Uamuzi huo wa Baraza la Seneti ulisababisha maandamano yaliyogharimu maisha ya mtu mmoja na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Baada ya hali hiyo mazungumzo ya kisiasa yalianzishwa kati ya vyama vya kisiasa mbalimbali, chini ya uangalizi wa Kanisa Katoliki nchini humo, lakini upinzani ulijiondoa baadae katika mazungumzo hayo.