Ziara ya wasuluhishi kwenda Gambia yaahirishwa
Wasuluhishi kutoka katika baadhi ya nchi za Afrika waliokua wanatazamiwa kwenda Gambia Jumatano hii Januari 11 wameahirisha ziara hiyo kutokana na ombi la rais Yahya Jammeh.
Imechapishwa:
Wasuluhishi hao wanajaribu kutatua mgogoro wa kisiasa nchini Gambia , baada ya rais Jammeh kukataa kung'atuka madarakani akidai kuwa uchaguzi wa urais uliyofanyika mwezi Desemba 2016 uligubikwa na kasoro.
Hata hivyo chanzo kilio karibu na wasuluhishi hao kimesema kuwa viongozi hao kutoka Afrika watakwenda nchini Gambia siku ya Ijumaa.
Wakati huo huo viongozi wa nchi za Afrika Magharibi wamemtaka rais Jammeh kuachia ngazi, huku wakisema kuwa watahudhuria sherehe za kuapishwa kwa kiongozi wa upinzani Adama Barrow baadae mwezi huu.
Awali, Waziri wa habari wa Gambia alisema iwapo Adama Barrow ataapishwa itakuwa kinyume cha katiba kwani kesi iliyowakilishwa mahakamani na rais Jammeh ya kupinga matokeo bado haijashughulikiwa.
Itakumbukwa kwamba Jumanne wiki hii mahakama kuu nchini Gambia iliahirisha kusikiliza kesi hiyo hadi mwezi Mei mwaka huu.