Baadhi ya vyama vya upinzani vyakataa makubaliano yaliyofikiwa na serikali
Masuala nyeti ya makubaliano yanayotazamiwa kusainiwa katika mazungumzo ya kitaifa, yaliyowekwa wazi kwenye RFI Jumamosi asubuhi na kuthibitishwa na kamati inayosimamia mazungumzo hayo siku hiyo hiyo baada ya mkutano uliyoendeshwa na msuluhishi Edem Kodjo, yatawasilishwa katika kikao kitakachowajumuisha wajumbe mia tatu Jumatatu hii mchana.
Imechapishwa:
Ni makubaliano ambayo yataendelea kuvipa fursa vyama vingine vya upinzani ambavyo vimekataa kushirki mazungumo hayo. Vyama hivi vya upinzani vinavyoongozwa na Etienne Tshisekedi pamoja na Moise Katumbi Chapwe, bila kusahau baadhi ya vyama vya kiraia wamefutilia mbali baadhi ya Ibara za nakala hii zinazoweka uchaguzi wa urais mapema mwishoni mwa mwezi Aprili 2018 na zinapendekeza kusalia mamlakani kwa Rais Joseph Kabila licha ya muhula wake wa pili na wa mwisho kumalizika, kwa mujibu wa katiba.
Vyama hivi vya upinzani vinaeleza kwamba huo ni mpango uliyoandaliwa chama tawala kikishirikiana na vyama vinavyokiunga mkono kwa lengo la kumbakiza madarakani Rais Joseph Kabila.
Jean-Marc Kabund, Katibu Mkuu wa chama cha UDPS, amesema kuwa wananchi wa DR Congo hawahusiki katika makubaliano yaliyofikiwa kati ya vyama vinavyoiunga mkono serikali na upinzani uliyoshiriki katika mazungumzo. "Wananchi wa DR Congo walitoa msimamo wao tarehe 19 na 20 Septemba 2016 na ninawaomba wananchi wa DR Congo kukataa kabisa mkataba huu na kuendelea kuomba mazungumzo ya kweli ambayo yataheshimu katiba yetu, ambayo yataheshimu uamuzi wa wananchi wa DR Congo ambao wanataka kuona nchi yao kukishuhudiwa suala la kupishana katika madaraka, " Bw Kabund ameiambia RFI.
Kwa upande wa vyama vya kiraia ambavyo havikushiriki katika mazungumzo, vinasema kuwa makubaliano hayo ni ukiukaji wa Katiba.