Carlo Ancelotti: Brazil inatafuta huduma zangu
NAIROBI – Kocha wa Real Madrid Carlo Ancelotti amedhibitisha kua taifa la Brazil lina nia ya kumuajiri kazi kama kocha Mkuu wa timu yao ya Taifa.
Imechapishwa:
Ancelotti raia wa Italia, amesema shirikisho la soka Brazil linamtaka kujaza nafasi iliyowachwa wazi na Adenor Leonardo Bacchi almaarufu Tite.
"Ndiyo, ukweli ni kwamba timu ya taifa ya Brazil inanitaka, naipenda na inanifurahisha," Ancelotti alisema katika mkutano na waandishi wa habari za michezo.
Mwalimu Tite aliacha nafasi hii baada ya Brazil maarufu ‘the Selecao's’ kuondolewa katika Kombe la Dunia la 2022 kwenye robo fainali.
Kandarasi ya Kocha Ancelotti na Real Madrid imebaki mwaka mmoja kwani inafika mwisho mwezi juni mwaka ujao 2024, akisema kua yupo tayari kuendelea kuitumikia.
Madrid kwa sasa wanashikilia nafasi ya pili kwenye msimamo wa La Liga, wakiwa nyuma ya vinara Barcelona kwa pointi 12.
"Kwa upande wangu, ni rahisi sana. Nina mkataba na ninataka kuuona, kwa sababu napenda Real Madrid, napenda klabu hii na chochote kinachoweza kutokea baada ya hapo ni mambo ya siku zijazo, na hakuna anayejua maisha ya baadaye." aliongeza Ancelotti.
Kikosi cha Ancelotti kitawakaribisha Real Valladolid hapo kesho Jumapili kwenye ligi ya daraja la kwanza kabla ya kumenyana na Barcelona katika mechi ya mkondo wa pili wa nusu fainali ya Copa del Rey Jumatano.
Timu ya Taifa ya Brazil kwa sasa inaongozwa na Ramon Menezes akisimamia kwa muda.