Kriketi: Kocha wa Australia kujiuzulu nafasi yake baada ya kashfa
Kocha wa timu ya taifa ya mchezo wa kriketi ya Australia Darren Lehmannn amesema atajiuzulu nafasi yake baada ya mchezo wa mzunguko wa nne na wa mwisho wa mfululizo wa mechi za mchezo huo nchini Afrika Kusini.
Imechapishwa:
“Huu utakuwa mchezo wangu wa mwisho kama kocha mkuu wa timu ya kriketi ya Australia,” amesema Lehmannn kwenye mkutano wake na wanahabari kuelekea mchezo huo.
“Kusema kwaheri kwa wachezaji ilikuwa ni kitu kigumu sana kwangu kukifanya.”
Lehmannn ambaye alitakiwa kuifundisha timu hiyo hadi mwishoni mwa msimu wa mwaka 2019 nchini Uingereza, anaachia ngazi licha ya kusafishwa kutokana na kashfa ya kujaribu kuuchezea mpira iliyoibusha hisia kali.
Uamuzi wake umekuja baada ya adhabu ya miezi 12 aliyopewa nahodha wa timu ya taifa ya Australia Steve Smith na naibu nahodha David Warner kwa namna walivyoshiriki udanganyifu jijini Capetown wakati wa mchezo wa mzunguko wa tatu Jumamosi iliyopita.
Mpigaji mipiria, Cameron Bancroft yeye amefungiwa kwa muda wa miezi 9 kwa kosa la kujaribu kuuharibu mpira.
Shirikisho la kimataifa la mchezo wa Kriketi linajiandaa kupitia adhabu za kuuharibu mpira wakati huu Australia ikikumbwa na kashfa ya udanganyifu, shikirikisho hili likionya kuwa mchezo uko hatarini hadi pale hatua stahiki zitakapochukuliwa.
Katika hatua nyingine nahodha wa timu ya taifa ya mchezo wa kriketi ya Afrika Kusini, Faf du Plessis amesema adhabu aliyopewa nahodha wa timu ya taifa ya Australia Steven Smith ilikuwa kali sana.
Smith na naibu wake David Warner walifungikiwa kwa miezi 12 huku Cameron Bancroft akifungiwa miezi 9 kwa kujaribu kuharibu mpira wakati wa mchezo wao na Afrika Kusini.