Jamhuri ya Czech yaangukia pua dhidi ya Uhispania
Timu ya taifa ya Uhispania imeanza vema michuano ya kombe la Ulaya mwaka huu inayofanyika nchini Ufaransa, baada ya kuchomoza na ushindi kwenye mchezo wake wa kwanza wa kundi D dhidi ya Jamhuri ya Czech.
Imechapishwa:
Uhispania inayonolewa na kocha mkongwe, Vicente del Bosque, iliwalazimu kusubiri hadi dakika za lala salama kuweza kupata bao la ushindi, ambalo sasa linaweka hai matumaini ya kusaka taji la mwaka huu.
Iliwachukua dakika 86 kwa Uhispania kuandika bao, lililofungwa na beki wa kati wa timu hiyo, Gerard Pique, aliyepokea pasi kutoka kwa kiungo mkongwe, Andres Iniesta.
Bao hili lilidumu hadi mwamuzi alipopuliza filimbi ya mwisho.
Uhispania hata hivyo inabidi wamshukuru mlinda mlango wao David De Gea aliyekuwa kizingiti kikubwa kwa washambuliaji wa timu ya taifa ya Jamhuri ya Czech ambao michomo yao haikuweza kufua dafu.
Kwa upande wa Jamhuri ya Czech wao, itabidi wajilaumu wenyewe kwa kukosa mabao mengi ya wazi ambayo kama washambuliaji wake wangekuwa makini pengine wangeweza kubadili mchezo.
Hata hivyo shukrani zimwendee mlinda mlango mkongwe, Peter Czech ambaye nae kwa sehemu kubwa ya mchezo, alikuwa kizingiti kwa washambuliaji wa Uhispania waliokuwa wakiachia michomo ambayo hata hivyo ilipanguliwa na kipa huyo.