Pata taarifa kuu
SOKA

Eto'o akubali kuichezea Cameroon baada ya rais Biya kuingilia kati

Rais wa Cameroon Paul Biya amemsihi mshambulizi wa timu ya taifa ya soka Samuel Eto'o kutostaafu kucheza soka la Kimataifa.

Matangazo ya kibiashara

Mshambulizi huyo wa Chelsea amekutana na wawakilishi wa rais Biya jijini Yaounde kujadiliana kuhusu hatima ya Eto'o ambaye tayari alikuwa ametangaza kustaafu kuichezea timu ya taifa.

Baada ya kikao hicho Eto'o alikubali kuichezea tena Cameoon na sasa atasafiri Ufaransa kujiunga na kikosi cha Indomitable Lions kinachojiandaa kumenyana na Tunisia katika mchuano wa kufuzu kwa kombe la dunia nchini Brazil mwaka 2014.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 32 baada ya mchuano wa makundi dhidi ya Libya aliwaambia wachezaji wenzake kuwa alikuwa amestaafu kucheza soka la Kimataifa.

Licha ya Eto kutoa tangazo hilo, kocha wa Cameroon Volker Finke alikuwa amemjumuisha katika kikosi chake cha mwisho.

Awali, Eto'o amekuwa na uhusiano mbaya na shirikisho la soka nchini Cameroon baada ya kuongoza mgomo wa wachezaji mwaka 2011 na kususia mchuano wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Algeria.

Hatua hiyo ilimsababishia kupewa adhabu ya kufungiwa mechi 15 na baadaye kupunguzwa hadi mechi nane baada ya kukata rufaa.

Licha ya adhabu yake kukamilikia Eto'o, alisusia kuichezea timu yake ya taifa kwa miezi kadhaa.

Mbali na Eto'o rais Biya pia aliwahi kumsihi mchezaji maarufu wa zamani Roger Milla kuicheza katika kombe la dunia mwaka 1990.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.