Hamas/Israeli: Rais Biden anamatumaini ya kupatikana muafaka kabla ya Ramadhan
Nairobi – Rais wa Marekani Joe Biden amesema anatarajia kupatikana kwa muafaka wa kusitisha vita kati ya wapiganaji wa Hamas na Israeli kabla ya kuanza kwa mwezi mtukufu wa Ramadhan.
Imechapishwa:
Kauli ya Biden imekuja wakati huu jamii ya kimataifa ikitoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi huru kufuatia hatua ya wanajeshi wa Israeli kutekeleza shambulio katika eneo la kutoa chakula cha msaada kwa raia wa Palestina kaskazini mwa mji wa Gaza.
Wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas inasema zaidi ya watu 100 waliuawa katika shambulio hilo.
Haya yanajiri wakati huu pia karibia raia 17 wa Palestina wameripotiwa kuuawa wakati wengine wakijeruhiwa katika shambulio la angani kwenye nyumba tatu katika maeneo ya Deir el-Balah na Jabalia.
Shirika la habari la Palestina Wafa wakati likinuku vyanzo vya katika idara ya afya limesema watu 15 wameuawa katika shambulio hilo kwenye nyumba mbili mashariki mwa Deir el-Balah katikati mwa Gaza.
Aidha taarifa hiyo pia imesema watu wengine wawili waliuawa kaskazini mwa Gaza katika kambi ya Jabalia baada ya ndege za kivita za Israeli kushambulia nyumba mbili.
Inadaiwa kuwa nyumba hiyo ilikuwa inatoa hifadhi kwa raia 70 wa Palestina waliopoteza makazi yao.
Katika upande mwengine, Maofisa wa usalama nchini Lebanon wanaripoti kuwa watu watatu wameuawa katika kile wanachodai ni shambulio la ndege zisizo na rubani za Israeli kusini wa Lebanon.
Mashambulio ya Israeli ya usiku kucha yalilenga maeneo kadhaa katika eneo la mpaka katika kijiji cha Blida.
Karibia wapiganaji wanne wa Hezbollah waliuawa katika mashambulio hayo.