Iran: Watu wenye silaha wawaua wageni tisa karibu na mpaka na Pakistan
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Iran, watu waliokuwa na silaha wamewaua watu tisa wasio Wairani kusini-mashariki mwa nchi siku ya Jumamosi, takriban siku kumi baada ya majibizano mabaya ya risasi kati ya Tehran na Islamabad.
Imechapishwa:
Watu wenye silaha wamewaua wageni tisa kwa kushambulia nyumba moja kusini mashariki mwa Iran siku ya Jumamosi, Januari 27, vyombo vya habari vya Iran vimesema, wiki moja baada ya makabiliano mabaya kati ya Iran na Pakistan katika eneo hili la mpakani lenye vurugu.
"Kwa mujibu wa mashahidi, watu waliokuwa na silaha waliwaua watu tisa wasio Wairani katika nyumba karibu na mji wa Saravan", katika mkoa wa Sistan-Baluchestan, liliripoti shirika la habari la Mehr, ambalo linabainisha kuwa hakuna kundi lolote lenye silaha hadi sasa limedai kuhusika na shambulio hilo, ambalo lilitokea asubuhi.
Tehran na Islamabad mara kwa mara zinashutumiana kila mmoja kwa kuyahifadhi makundi ya waasi na kuwawezesha kuanzisha mashambulizi katika maeneo yao.
Urushianaji risasi katikati ya mwezi wa Januari
Mnamo Januari 16, Iran ilifanya shambulio kwa kutumia makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya kundi la "kigaidi" katika eneo la Pakistan, ambalo lilijibu mnamo Januari 18 kwa kulenga "maficho ya kigaidi" nchini Iran. Mashambulizi haya mawili yalisababisha vifo vya watu 11, hasa wanawake na watoto, kulingana na mamlaka.
Mashambulizi hayo yamelisababisha mzozo mfupi wa kidiplomasia, huku Pakistan ikiwa imemwita balozi wake mjini Tehran na kutangaza kwamba balozi wa Iran nchini Pakistan, ambaye alikuwa nchini mwake, atazuiwa kurejea Islamabad.
Lakini nchi hizo mbili kisha zilitangaza, Januari 22, kurejea katika hali ya kawaida katika uhusiano wao na ziara ijayo ya mkuu wa diplomasia ya Iran Hossein Amir-Abdollahian katika mji mkuu wa Pakistan.
Mashambulio haya ya anga yalisababisha wasiwasi katika jumuiya ya kimataifa wakati ambapo Mashariki ya Kati inatikiswa na vita kati ya kundi la Kiislamu la Palestina, Hamas, na Israel katika Ukanda wa Gaza.
Pamoja na AFP