HRW: Mamia ya wahamiaji wa Ethiopia waliuawa na Saudi Arabia kwenye mpaka na Yemen
Shirika lisilo la kiserikali la Human Rights Watch linawatuhumu walinzi wa mpaka wa Saudia kwa kuwaua mamia ya wahajiri wa Ethiopia tangu mwaka jana waliokuwa wakijaribu kuingia Saudi Arabia kupitia mpaka wake na Yemen.
Imechapishwa:
Katika ripoti ya kurasa 73, Human Rights Watch inalaani hali inayowakabili mamia kwa maelfu ya Waethiopia wanaotumia "njia ya mashariki" inayounganisha Pembe ya Afrika na Ghuba, kupitia Yemen.
Shirika hilo lisilo la kiserikali linajikita kwenye mahojiano na wahamiaji 38 waliojaribu kuingia Saudi Arabia kutoka Yemen. Wanataja "silaha za vilipuzi", kufyatuliwa risasi kiholela kutoka kwa walinzi wa mpaka wa Saudi Arabia ambao waliwauliza Waethiopia "ni sehemu gani ya miili yao wangependelea kupigwa risasi". Walionusurika wanasimulia jinsi walivyopelekwa kwenye kambi za kizuizini, wakipigwa mawe. Kijana mmoja anadai alilazimishwa kuwabaka wasichana wawili wa umri wa miaka 15 ili kuepuka kunyongwa.
Picha za satelaiti, video na picha zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii "au zilizokusanywa kutoka vyanzo vingine" zinaunga mkono ushuhuda wa Waethiopia. Unaweza kuona watu wakikimbia kupitia milimani, wengine wamejeruhiwa. Hawa ni wahamiaji wa Ethiopia ambao waliondoka nchini mwao kwa sababu za kiuchumi au kwa sababu walihisi wako hatarini, kulingana na Human Right Watch.
Saudi authorities are spending billions on sports-washing to improve their image.
— Human Rights Watch (@hrw) August 21, 2023
But out of public view, Saudi border guards have killed at least hundreds of Ethiopian migrants and asylum seekers, including women and children, who tried to cross the Yemen-Saudi border. pic.twitter.com/1XmJavfxWI
Mamlaka ya Saudi inapinga tukio hilo lililoripotiwa na Human Right Watch. "Madai katika ripoti ya Human Rights Watch kwamba walinzi wa mpaka wa Saudi Arabia waliwafyatulia risasi Waethiopia waliokuwa wakivuka mpaka wa Saudi Arabia na Yemen hayana msingi na hayatokani na vyanzo vya kuaminika," chanzo cha serikali ya Saudi Arabia kimeliambia shirika la habari la AFP.
Mauaji "ya jumla na yaliyopangwa" ya wahamiaji wa Ethiopia yanaweza hata kujumuisha uhalifu dhidi ya binadamu, HRW imesema.
Mwaka jana, Umoja wa Mataifa uliripoti kitendo cha ufyatuaji wa mizinga na risasi za bunduki ndogo kwene mpaka, kitendo kilichotekelezwa na vikosi vya usalama vya Saudia na kuua wahamiaji 430 kusini mwa Saudi Arabia na kaskazini mwa Yemen katika kipindi cha miezi minne ya kwanza ya mwaka 2022.