Tetemeko la ardhi nchini Syria: Damascus yakubali kufungua vituo viwili vya mpaka na Uturuki
Rais wa Syria amekubali kufungua vituo viwili vipya vya mpaka kati ya Uturuki na kaskazini-magharibi mwa Syria kwa muda wa miezi mitatu ili kuwasilisha misaada ya kibinadamu kwa wahanga wa tetemeko la ardhi.
Imechapishwa:
Bashar al-Assad ametangaza uamuzi huo kwa mkuu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu Martin Griffiths ambaye alikutana naye mapema siku ya Jumatatu mjini Damascus. "Nakaribisha uamuzi wa Rais wa Syria Bashar al-Assad leo wa kufungua vivuko viwili vya Bab Al-Salam na Al Ra'ee kati ya Uturuki na kaskazini-magharibi mwa Syria kwa muda wa miezi mitatu," Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema katika taarifa yake. Washington pia imekaribisha kwa haraka tangazo hili, ikiwa litafuatiliwa vyema.
Wiki moja baada ya maafa hayo, Bashar al-Assad pia aliomba msaada wa kimataifa wa kujenga upya sehemu za nchi yake zilizoharibiwa na tetemeko la ardhi lililoua takriban watu 3,688 nchini Syria.
Watu milioni 4 walioathirika
Ufunguzi wa vituo viwili vipya vya mpakani "utawezesha misaada zaidi kuingia, kwa kasi", alifurahi Antonio Guterres. Kabla ya tetemeko hili la ardhi, karibu misaada yote muhimu ya kibinadamu kwa zaidi ya watu milioni 4 wanaoishi katika maeneo ya waasi kaskazini-magharibi mwa Syria ilisafirishwa kutoka Uturuki kupitia kivuko cha Bab al-Hawa, kituo pekee kilichoidhinishwa na Baraza la Usalama.
Utaratibu huu wa kuvuka mpaka ulioundwa mwaka 2014 na azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa unapingwa na Damascus, lakini pia na Moscow, mwanachama wa kudumu ambaye ana haki ya kura ya turufu na ambayo imeshawishi katika miaka ya hivi karibuni kupunguza idadi ya vituo vinne hadi kimoja.
Wito wa kufunguliwa kwa vivuko vingine ulitolewa katika siku za hivi karibuni, na wajumbe kadhaa wa Baraza la Usalama - Marekani, Ufaransa, Uingereza - walietoa wito wa azimio juu ya suala hilo. Lakini makubaliano ya Damascus yanafanya azimio hili kutotekelezwa.
(Pamoja na AFP)
Β