Yemen: zaidi ya watoto 11,000 waliuawa, kukatwa viungo vyao au kujeruhiwa tangu 2015
Yemen imeharibiwa na vita kati ya kundi la Houthi, waasi wanaoungwa mkono na Iran, na vikosi vinavyounga mkono serikali inayoungwa mkono na Saudi Arabia.
Imechapishwa:
Zaidi ya watoto 11,000 wameuawa, kukatwa viungo vyao au kujeruhiwa nchini Yemen tangu mwaka 2015 na karibu 4,000 wamejumuishwa katika vita vilivyoikumba nchi hiyo kwa zaidi ya miaka minane, Umoja wa Mataifa umetangaza Jumatatu.
Yemen ambayo ni nchi maskini zaidi kwenye Rasi ya Uarabuni, imeharibiwa tangu mwaka 2014 na mzozo kati ya Wahouthi, waasi wanaoungwa mkono na Iran, na vikosi vinavyounga mkono serikali inayoungwa mkono na muungano wa kijeshi unaoongozwa na nchi jirani ya Saudi Arabia.
Miongoni mwa waathiriwa wadogo 11,019, 3,774 walikufa, limesema Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Watoto (UNICEF) katika taarifa yake kwa vyombo vya habari.
Tathmini ya awali ya shirika la Umoja wa Mataifa iliripoti zaidi ya watoto 10,200 waliouawa, kujeruhiwa au kukatwa viungo vyao.
Takwimu zake mpya, zinazojumuisha kipindi cha kuanzia mwezi wa Machi 2015 hadi Septemba 30, 2022, zinazingatia tu kesi zilizothibitishwa na shirika hili.
Katika kipindi hiki, watoto 3,995 waliajiriwa: wavulana 3,904 kushiriki katika mapigano na wasichana 91 katika vituo vya ukaguzi au kushiriki katika baadhi ya matukio.