Iran yaruhusu Umoja wa Mataifa kutembelea maeneo mawili ya nyuklia
Hatimaye Iran imewaruhusu wakaguzi wa Shirika la kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA, kutembelea maeneo mawili ya nyuklia yanayoshukiwa kuhifadhi au kutumia vifaa vya nyuklia.
Imechapishwa:
Ruhsa hiyo inatolewa wakati ambapo mkurugenzi wa shirika hilo la Umoja wa Mataifa Rafael Grossi, anahitimisha ziara yake mjini Tehran.
Ridhaa hii ya Iran pia inakuja wakati kunaripotiwa mivutano inayohusiana na na jaribio la Marekani la kutaka kurefushwa kwa vikwazo vya Umoja wa Mataifa dhidi ya Tehran. Lakini Washington ilipata tena pigo kubwa Jumanne wiki hii mbele ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kujikuta pendekezo lake hilo linapingwa na karibu wajumbe wote wa baraza hilo.
"Iran imekubali kuruhusu Shirika la kimataifa la Nguvu za Atomiki, IAEA, kutembelea maeneo mawili yanayoshukiwa kuhifadhi au kutumia vifaa vya nyuklia," IAEA na mamlaka ya Nishati ya Atomiki ya Iran (OIEA) yamebaini Jumatano katika taarifa ya pamoja.
"Tumeafikiana tarehe za kutembelea maeneo hayo na shughuli za ukaguzi za IAEA ," mashrika hayo yameongeza, bila hata hivyo kutangaza tarehe rasmi.
Iran imekuwa ikipinga ukaguzi wa maeneo hayo, yanayoaminika kuwa ni ya kutoka mwanzoni mwa mwaka 2000, kabla taifa hilo halijasaini mkataba wa nyukilia wa mwaka 2015 na nchi zilizo na nguvu duniani, ikisema IAEA haikuwa na mamlaka ya kuyatembelea.