Coronavirus: Kesi ya kwanza ya maambukizi yaripotiwa katika kambi ya wakimbizi wa Palestina Lebanon
Kesi ya kwanza ya maambukizi ya virusi vya Corona imethibitishwa katika kambi ya wakimbizi wa Palestina katika bonde la Bekaa, Mashariki mwa Lebanon, Umoja wa Mataifa umetangaza.
Imechapishwa:
Umoja wa Mataifa umebaini kwamba vipimo vitafanywa kwa wakazi wa eneo hilo.
Mgonjwa huyo amesafirishwa katika hospitali ya umma ya Rafic Hariri, jijini Beirut, limesema shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi wa Palestina (UNRWA), ambalo halikutoa habari yoyote juu ya umri wake au hali yake ya afya.
Kulingana na chanzo hicho, mgonjwa huyo ni mkimbizi kutoka Palestina anayeishi nchini Lebanon baada ya kuhama kutoka nchi jirani ya Syria, inayokumbwa na machafuko mabaya kwa karibu muongo mmoja.
Amekuwa anaishi katika kambi ya Wavel - inayojulikana zaidi kwa Kiarabu kama "kambi ya Galilaya" - karibu na Baalbek, huko Bekaa.
Timu ya wataalam wa matibabu wanatarajia kuzuru kambi hiyo leo Jumatan ili "kufanya vipimo" vya damu kwa uchunguzi kuhusu ugonjwa Covid-19, kulingana na taarifa kutoka Unrwa.
Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi wa Palestina (UNRWA) litafanya kile kinachohitajika "kusaidia familia ya mgonjwa huyo kujitenga katika nyumba yao," taarifa hiyo imeongeza. Mgonjwa atatibiwa kwa gharama ya UNRWA.