Askari wanne wa Uturuki wauawa katika mapigano Idleb, Syria
Wanajeshi wanne wa Uturuki wameuawa na tisa kujeruhiwa Jumatatu hii, Februari 3, baada ya jeshi la Syria kurusha makombora katika Jimbo la Idleb Kaskazini Magharibi mwa Syria.
Imechapishwa:
Taarifa hii imetolewa leo asubuhi na Wizara ya Ulinzi ya Uturuki, ambayo inasema kwamba jeshi la Uturuki limejibu na "kuharibu mitambo kadhaa ya jeshi la Syria".
Kuongezeka kwa uhasama huu kunakuja baada ya Syria na Urusi kutekeleza mashambulizi kwa miezi kadhaa dhidi ya Jimbo la Idleb, jimbo ambalo mpaka sasa halijadhibitiwa na jeshi la rais Bashar al-Assad.
Wengi walionya kuwa kuna hatari ya kutokea mapigano kati ya jeshi la Uturuki na lile la Syria katika Jimbo la Idleb.
Vikosi vya Bashar al-Assad, vilizindua mashambulizi tangu mwezi Aprili 2019 kwa lengo la kuweka Jimbo la Idleb kwenye himaya yake.
Kulingana na Wizara ya Ulinzi ya Uturuki, askari wake wamelengwa na shambulio hilo la jeshi la Syria, bila hata hivyo kutaja eneo ambalo mapigano hayo yalitokea.
Tangu Urusi na Uturuki kutia saini kwenye makubaliano mwezi Septemba 2018, jeshi la Uturuki lipo Idleb kwenye ngome 12.