Shirika la Msalaba mwekundu lashindwa kuwafikia waathiriwa wa vita Mashariki mwa Ghouta
Shirika la Kimataifa la Msalaba mwekundu linasema, misaada ya kibinadamu haitawafikia waathiriwa wa vita Mashariki mwa Ghouta siku Alhamisi nchini Syria.
Imechapishwa:
Hii inatokana na vita vinavyoendelea katika ngome hiyo ya upinzani kwa mujibu wa msemaji wa Shirika hilo Ingy Sedky.
Wiki hii ,malori 46 yaliyobeba misaada ya kibinadamu yaliingia katika ngome hiyo ya upinzani lakini, maelfu ya watu hawakupata msaada kwa sababu ya kuendelea kwa mashambulizi.
Siku ya Jumatano pekee, mashambulizi dhidi ya wapiganaji wa upinzani yalisababisha vifo vya watu 45, katika ngome hiyo iliyo karibu na mji mkuu wa Damascus.
Waangalizi wa mzozo huu wanasema watoto wanne ni miongoni mwa watu waliopoteza maisha katika mashambulizi haya yanayoendelea.
Takwimu kutoka kwa Mashirika ya kutetea haki za binadamu zinaonesha kuwa watu zaidi ya 600 wamepoteza maisha Mashariki mwa Ghouta, kwa kipindi cha mwezi mmoja uliopota.