Jeshi la Syria lashambulia tena mji wa Allepo, wakaazi wakwama
Serikali ya Syria imeanza tena kushambulia Mashariki mwa mji wa Allepo nchini Syria, saa chache baada ya mkataba wa kusitisha mapigano hayo kufikiwa.
Imechapishwa:
Waangalizi wa mzozo wa Syria wanasema ndege za kijeshi zimeonekana zikishambulia wilaya kadhaa ya mji huo na kuhatarisha maisha ya wakaazi wa mji huo.
Mashambulizi haya mapya yamekuja baada ya mkataba huo kutaka wakaazi wa Allepo kuondolewa na kwenda katika maeneo salama.
Mabasi ya serikali yalionekana katika mji huo tayari kuwaondoa watu hao lakini hakuna kilichofanyika kwa mujibu wa waangalizi ambao ni watetezi wa Haki za Binadamu.
Mashariki mwa mji wa Allepo ndilo eneo ambalo limekuwa ngome ya waasi tangu mwaka 2012 na serikali ya Syria kwa usaidizi wa wanajeshi wa Urusi imekuwa ikishambulia ngome hiyo.
Umoja wa Mataifa nao unasema kuwa una ushahidi wa mashambulizi hayo kusababisha mauaji makubwa na ukiukwaji mkubwa wa haki za kibinadamu.
Hatima ya wakaazi wa mji huo sasa haifahamiki.