Saudi Arabia yamnyonga kiongozi wa kidini, Iran yalaani
Saudi Arabia imewanyonga watu 47 Jumamosi hii waliohukumiwa kwa kosa la "ugaidi", ikiwa ni pamoja na kiongozi wa kidini kutoka jamii ya Mashia, Nimr Baqir al-Nimr, kiongozi wa kundi linaloipinga serikali ya nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Hali hiyo imezua hasira katika jamii ya Mashia ulimwenguni.
Miongoni mwa watu wengine 46 walionyongwa ni pamoja na wanajihadi wengi wa Al Qaeda, wakati ambapo utawala wa kifalme una wasiwasi kuhusu tishio la Masuni wenye msimamo mkali kama kundi la Islamic State (IS). Kundi la Al Qaeda hivi karibuni liliapa kulipiza kisasi iwapo wanamgambo wake watanyongwa.
Iran imeghadhabishwa na kitendo hicho cha kuuawa kwa Cheick al-Nimr. Mahusiano wakati huu kati ya Iran yenye Mashia wengi na Saudi Arabia yenye Masuni wengi yamedorora kwa kiasi kikubwa. Tehran imeionya Riyadh kuwa itajutia kifo hicho, wakati ambapo maandamano yameitishwa nchini Iran kufanyika Jumapili dhidi ya Saudi Arabia.
Akiyakosoa maeneno ya serikali ya Tehran, msemaji wa Wizara ya mambo ya ndani ya Saudi Arabia, Mansour al-Turki, amesema nchi yake "haitishwi na fikra za wengine."
Watu walionyongwa, ikiwa ni pamoja na raia 45 wa Saudi Arabia, raia mmoja kutoka Misr na mmoja kutoka Chad wameuawa kwa upanga au kwa kupigwa risasi katika miji kumi na miwili ya Saudi Arabia.
Walikuwa wamehukumiwa, kwa mujibu wa serikali ya Saudi Arabia, katika kesi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kujiunga na itikadi yenye msimamo mkali, kutoka "makundi ya kigaidi".
Tawala za kifalme kutoka jamii ya Masuni katika Ukanda huo, ikiwa ni pamoja na Bahrain na Umoja wa Falme za Kiarabu zimekaribisha mtizamo wa Saudi Arabia. Nchini Bahrain, baadhi ya vijana wa Kishia walio wengi, hata hivyo, wamekusanyika katika kitongoji cha Manama kupinga mauaji hayo.