Mahakama kuu yaagiza wakili wa upinzani kuruhusiwa kurejea Kenya
Mahakama Kuu ya Kenya imeagiza mwanasiasa wakili wa upinzani Miguna Miguna aliyetimuliwa nchini humo mapema mwezi huu aruhusiwe kurejea nchini.
Imechapishwa:
Bw Miguna alikamatwa na polisi kwa mchango wake katika kuapishwa kwa Bw Odinga kuwa "rais wa wananchi", hafla iliyofanyika uwanja wa Uhuru Park, Nairobi mnamo 30 Januari.
Bw Miguna, ambaye pia ni wakili, ndiye aliyetia saini hati ya kiapo ya Bw Odinga.
Serikali ilikuwa imeeleza hatua hiyo ya kiongozi huyo wa upinzani kuwa uhaini wa hali ya juu.
Bw Miguna, alikuwa mshauri wa kiongozi wa upinzani Raila Odinga alipokuwa waziri mkuu wa nchi hiyo. Aliondolewa nchini humo na kupelekwa Canada baada ya kuzuiliwa kwa siku kadhaa.
Mahakam kuu imeamuru serikali kumpa Bw Miguna Miguna hati za kusafiria za kumuwezesha kurejea Kenya na kuhakikisha anasalia nchini humo hadi kesi yake dhidi ya serikali ikamilike kusikizwa.
Kabla yakuondolewa kwake mchini Kenya kwa nguvu mnamo 7 Februari, serikali ilikuwa imekataa maagizo ya kumuwasilisha Bw Miguna mahakamani mara kadha.
Wakati wa kutimuliwa kwake, alipokonywa paspoti yake ya Kenya hali iliyopunguza uwezekano wake wa kurejea Kenya kama Mkenya.