Kenya yalaani ripoti ya EU kuhusu uchaguzi
Serikali ya Kenya imekashifu vikali ripoti ya waangalizi wa uchaguzi kutoka umoja wa Mataifa ikisema ripoti hiyo haikuwa na nia njema kwa Serikali na imetolewa kabla ya muda.
Imechapishwa:
Mkuu wa ujumbe wa waangalizi wa umoja wa Ulaya Marietji Schaake ambaye alilazimika kutoa ripoti hiyo akiwa mjini Brussels badala ya Kenya, amesema uchaguzi uliharibiwa na wanasiasa wa pande zote mbili huku wapiga kura wakihongwa pesa na taasisi huru kuingiliwa kwenye maamuzi yake.
Schaake ameongeza kuwa wamelazimika kuichapisha ripoti hiyo wakiwa nje ya nchi kutokana na Serikali ya Kenya kutokuwa tayari kuwapokea wala kukubali kuchapishwa kwa ripoti hiyo.
Marietji Schaake amesema wananchi wa Kenya wamegawanyika kutokana na uchaguzi mkuu uliopita.
Serikali ya Kenya kupitia ubalozi wake mjini Brussels, nchini Ubelgiji imesema kuwa madai hayo sio ya ukweli na kwamba ujumbe wa EU ulikiuka makubaliano kati ya taifa hilo na EU
Waangalizi wa Umoja wa Ulaya, walioshuhudia Uchaguzi Mkuu nchini Kenya mwezi Agosti na Oktoba mwaka uliopita, katika ripoti yao ya mwisho wamesema, Uchaguzi huo ulitawaliwa na rushwa, matumizi ya rasilimali za umma hasa kwa viongozi wa chama tawala Jubilee.
Ripoti hiyo imeorodhesha pia mapendekezo zaidi ya 29 ikiwemo kufanyika kwa mabadiliko ya sheria za uchaguzi, kuimarishwa kwa tume ya uchaguzi na kuboreshwa kwa mfumo wa kielektroniki utakaowezesha kuwa na uchaguzi huru mwaka 2022 wakati rais Uhuru Kenyatta atakapotakiwa kuondoka madarakani.