Pata taarifa kuu
UGANDA-WABUNGE

NRM yawasilisha mswada kubadilisha Katiba huku wabunge wakipigana

Wabunge wa chama tawala nchini Uganda wamefanikiwa kuwasilisha ombi la kuandaa mswada wa kubadilisha katiba na kuondoa kifungu kinachozuia mtu kuwania urais akiwa na umri wa zaidi ya miaka 75.

Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, akizungumza wakati wa mkutano wa mawaziri na makatibu wakuu wa wizara nchini humo, 31 Julai, 2016
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, akizungumza wakati wa mkutano wa mawaziri na makatibu wakuu wa wizara nchini humo, 31 Julai, 2016 NRM Photo
Matangazo ya kibiashara

Hatua hii imekuja baada ya Spika wa Bunge Rebecca Kadaga kuwafukuza bungeni 25 wa upinzani kwa kile alichosema walikosa nidhamu.

Wabunge hao pamoja na kupewa adhabu hiyo, watakosa vikao vitatu vya bunge.

Punde tu baada ya uamuzi huo, makabiliano makali yalizuka huku wabunge wa upinzani wakipigana na wenzao wa chama tawala lakini pia maafisa wa usalama waliokuja bungeni kuwaondoa nje.

Wabunge wa upinzani walionekana wakipanda juu ya viti na meza ya bunge na kuharibu vipaza sauti.

Baada ya mvutano huo uliodumu kwa zaidi ya saa moja, mbunge wa NRM Raphael Mugyezi aliomba nafasi ya kuandaa mswada huo.

“Mswada huu unawasilishwa ili kuliomba bunge hili kuniruhusu niandae mswada maalum ili usomwe hapa bungeni,” amesema Raphael Magyezi

'Mheshimiwa Spika, naomba muunge mkono mswada huu wa kibinafsi ili niende niuandae usomwe,” aliongeza.

Wakati wa uwasilishwaji wa ombi hilo, wabunge wote wa upinzani walikuwa nje huku NRM wakisalia peke yao.

Hata hivyo, upinzani wameapa kuendelea kupambana kuhakikisha kuwa mabadiliko hayo hayafanyiki.

Wabunge wa NRM wanasema, mabadiliko hayo yanatoa fursa kwa raia yeyote wa nchi hiyo kuwania urais bila kuangalia umri wake.

Ikiwa Katiba itabadilishwa, rais Yoweri Museveni mwenye umri wa miaka 72 atawania urais mwaka tena mwaka 2021 baada ya kuongoza kwa zaidi ya miaka 30.

Raia wa Uganda hawakupata nafasi ya kushuhudia kilichokuwa kinaendelea baada ya Tume ya Mawasiliano nchini humo kupiga marufuku kuoneshwa moja kwa moja kwa vikao vya bunge kwa madai kuwa inawachochea wananchi.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.