Tanzania yazindua mradi wa ujenzi wa reli ya kati
Tanzania imezindua mradi wa ujenzi wa reli ya kati katika harakati za kuimarisha sekta ya uchukuzi nchini humo.
Imechapishwa:
Awamu ya kwanza ya ujenzi wa reli hiyo itatoka jijini Dar es salaam kwenda mjini Morogoro umbali wa Kilomita 205.
Treni ya abiria inatarajiwa kusafiri kwa mwendo wa Kilomita 160 kwa saa, kwa sababu inatarajiwa kutumia umeme katika reli hiyo mpya.
Awamu ya kwanza ya mradi huu itaigharimu serikali ya Tanzania Dola za Marekani Bilioni 1.22, ujenzi ambao unatarajiwa kumalizika baada ya miezi 30.
Serikali ya Tanzani inasema fedha za mradi huo itapatikana kupitia mkopo kutoka mashirika mbalimbali ya kimataifa ya kifedha.
Kandarasi ya kufanikisha mradi huu imetolewa kwa kampuni ya Yapi Merkez ya Uturuki na Mota-Engil ya Ureno zinazoshirikiana.
Baada ya awamu ya kwanza kumalizika, ujenzi wa Kilomita 1,216 ya reli hiyo itaendelea kuelekea miji mingine ya nchi hiyo na kuunganisha mataifa jirani ya Rwanda na Burundi ili kufanikisha mradi wa reli katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Rais John Magufuli amesema mradi huu unatarajiwa, kutoa nafasi za kazi kwa Watanzania lakini pia kusaidia kuimarisha sekta ya uchukuzi na kuinua uchumi wa nchi hiyo baada ya kukamilika.
Kenya tayari imemaliza awamu ya kwanza ya ujenzi wa reli ya kati kutoka Mombasa hadi jiji kuu la Nairobi, umbali wa Kilomita 485.
Kenya imetumia Dola za Marekani Bilioni 3.6 kufanikisha ujenzi huu na matumizi ya reli hii yanatarajiwa kuanza tarehe 1 mwezi Juni kuwasafirisha abiria na mizigo kutoka.
Mradi huo wa 1,435 unatarajiwa kuunganisha Kenya, Uganda na Sudan Kusini.