Wanajeshi wa Kenya waanza kurejea nyumbani kutoka Sudan Kusini
Serikali ya Kenya imeanza zoezi la kuwarudisha nyumbani wanajeshi wake wa ambao wanalinda amani nchini Sudan Kusini chini ya mwavuli wa Umoja wa Mataifa.
Imechapishwa:
Kundi la kwanza la wanajeshi 100 kati ya 1000 ambao wamekuwa nchini humo waliwasili jijini Nairobi siku ya Jumatano.
Wakuu wa jeshi nchini humo wanasema wengine 100 wanawasili siku ya Alhamisi, na wataendelea kurudi nyumbani kwa makundi hadi pale watakapomalizika nchini humo.
Hatua hii ya Kenya imekuja baada ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon kumfuta kazi Kamanda wa majeshi hayo ya kulinda amani ambaye ni raia wa Kenya Luteni Jenerali Johnson Ondieki.
Moon alimshutumu Kamanda huyo kwa kushindwa kuzuia mauaji dhidi ya raia baada ya kuzuka kwa mapigano makali kati ya waasi na wanajeshi wa serikali jijini Juba.
Kenya inasema kuachishwa kazi kwa kamanda wake hakutasaidia kumaliza mzozo wa Sudan Kusini, huku Umoja wa Mataifa na serikali ya Juba ikiiomba serikali ya Kenya kuachana na mpango wa kuwarudisha nyumbani wanajeshi wake.