DRC: M23 watishia kuchukua tena maeneo waliyokabidhi vikosi vya EAC.
Nairobi – Kundi la waasi wa M23 linaloendelea kutatiza usalama mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, limetishia kuchukua tena udhibiti wa maeneo ambayo lilikuwa limepokeza kwa vikosi vya Jumuiya ya Afrika Mashariki, punde tu vitakapoondoka nchini humo.
Imechapishwa:
Tangazo la kundi hilo linakuja baada ya vikosi hivyo siku ya Jumamosi, Disemba 2, kuanza kuondoka mkoa wa Kivu Kaskazini, miezi kadhaa kupita tangu Kinshasa ivituhumu kushindwa kutumiza majukumu yake.
Kufuatia kuondoka kwa vikosi vya EACRF kutoka DRC, M23 itachukua tena maeneo yake yote ambayo ilikabidhi kwa EACRF mwanzoni mwa mchakato wa amani, msemaji wa kundi la waasi Lawrence Kanyuka alisema katika taarifa siku ya Jumapili.
Vikosi hivyo vinavyojumuisha wanajeshi kutoka Kenya, Burundi, Uganda, na Sudan Kusini, vilitumwa nchini humo mwezi Novemba mwaka 2022, ili kuchukua nafasi zilizokaliwa na M23 ili kuruhusu mchakato wa amani kuendelea.
Hata hivyo, serikali ya Kinshasa imesema kuwa haitaongeza muda kwa vikosi hivyo kuendelea kuhudumu nchini humo baada ya Disemba 8, rais Felix Tshisekedi, akivishutumu vikosi hivyo kwa kuishi pamoja na waasi badala ya kuwalazimisha kuweka silaha chini.
Kundi la kwanza la wanajeshi 100 wa Kenya kutoka katika kikosi hicho, waliondoka kutoka uwanja wa ndege wa Goma kuelekea Nairobi, kulingana na msemaji wa kikosi hicho ambaye hakutoa maelezo zaidi.
Vikosi vya kulinda amani kuondoka
Mnamo mwezi Mei mwaka huu, rais Tshisekedi alitishia kukiondoa kikosi cha kikanda nchini humo baada ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) kuidhinisha ujumbe wa kijeshi katika eneo la mashariki linalokumbwa na migogoro, na kikosi cha SADC kilitarajiwa kuwasili nchini humo kabla ya mwisho wa mwezi Disemba.
Eneo la Mashariki mwa DRC, limekuwa nyumbani kwa zaidi ya makundi 130 yenye silaha, na kutatiza usalama kwa takriban miongo mitatu, wakati huu pia utawala wa Kinshasa ukiutaka ujumbe wa kulinda amani wa umoja wa mataifa MONUSCO kuondoka nchini humo kufikia mwishoni mwa mwezi huu, wakituhumiwa kushindwa kumaliza miongo kadhaa ya ghasia.