Kampeni za kuelekea uchaguzi mkuu zinaendelea nchini DRC
Kinara mwingine wa upinzani nchini DRC, gavana wa zamani wa Katanga, Moise Katumbi, hapo jana alizindua rasmi kampeni zake za kuwania kiti cha urais kaskazini mwa mji wa Kisangani, wakati huu akiendelea kupata uungwaji mkono toka kwa wagombea wengine.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Aidha baada ya waziri mkuu wa zamani Matata Ponyo kujiondoa kama mgombea na kutangaza kumuunga mkono Katumbi, wagombea wengine Seth Kikuni na Frank Diongo nao wamefuata mkondo huo.
Wagombea wengine waliozindua kampeni zao ni pamoja na daktari Denis Mukwege na mwanamke pekee kwenye kinyang’anyiro hicho, Marie-Josee Ifoku, ambao wote wameahidi kupambana na vitendo vya rushwa na hali ya usalama ikiwa watachaguliwa.
Lakini Je kuungana kwao kutasaidia? Francois Alwende ni mchambuzi wa siasa za DRC anaangazia hili akiwa Kenya.
“Wapinzani wakitaka kupambana na rais Tshisekedi lazima wauungane lakini kuungana kwao siko jambo rahisi pia.” alieleza Francois Alwende.
Rais wa sasa Felix Tshisekedi anayewania kuchaguliwa kwa muhula wa pili, alizindua kampeni zake awali jijini Kinshasa kwenye uwanja wa Martyrs, ambapo aliahidi kukamilisha ahadi za uchaguzi na kusimamia usalama mashariki mwa nchi hiyo.
Mwingine aliyezindua kampeni zake siku ya Jumapili ni Martin Fayulu, ambaye alikuwa kwenye mji wa Bandundu, alikoahidi raia uwa atashughulikia changamoto zinazoikabili nchi kwa sasa, huku muwaniaji mwingine Delly Sesanga, akianza kampeni zake katika mkoa wa Kwango, wakati Seth Kikuni na Jean-Claude Baende wakianza kampeni yao huko Kinshasa.
Ni kampeni zinazotazamwa si tu na raia wa Congo lakini jumuiya ya kimataifa na waangalizi wa uchaguzi, ambao wametoa wito wa amani licha ya eneo la mashariki kukabiliwa na utovu wa usalama, hali inayozua maswali ikiwa baadhi ya maeneo ya mashariki mwa nchi hiyo yatafanya uchaguzi.