Pata taarifa kuu

Raia wa Rwanda ni wafungwa nchini mwao: Rusesabagina

Nairobi – Mkosoaji wa serikali ya Rwanda Paul Rusesabagina, ambaye alijipatia umaarufu kwa juhudi zake za kuwaokoa watu wakati wa mauaji ya kimbari ya mwaka wa 1994, amedai kuwa raia wa Rwanda ni wafungwa katika nchi yao.

Paul Rusesabagina amesema raia wa Rwanda ni wafungwa nchini mwao
Paul Rusesabagina amesema raia wa Rwanda ni wafungwa nchini mwao © Marvin Joseph/The Washington Post via Getty Image
Matangazo ya kibiashara

Katika ujumbe wake wa kwanza hadharani tangu kuachiwa huru kutoka jela nchini Rwanda mwezi Machi baada ya zaidi ya siku 900 gerezani, Rusesabagina aliishukuru Marekani kwa kuongoza mchakato wa kuachiwa kwake kutoka katika kile alichokitaja kama "kuzimu".

Aidha ameeleza kuwa ujumbe wake wa video kwenye mtandao wa YouTube ulitolewa ili kuendana na tangazo la uhuru wa Rwanda Julai 1, 1962.

"Kwa bahati mbaya leo, miaka 61 baadaye, Wanyarwanda bado hawapo huru. Wanyarwanda ni wafungwa ndani ya nchi yao," alisema Rusesabagina, akizungumza kutoka nyumbani kwake San Antonio katika jimbo la Texas nchini Marekani.

Paul Rusesabagina, alikuwa akizuiliwa nchini Rwanda kwa tuhuma za ugaidi
Paul Rusesabagina, alikuwa akizuiliwa nchini Rwanda kwa tuhuma za ugaidi © AP - Muhizi Olivier

"Rwanda ni serikali ya kimabavu ambayo haina haki kwa raia wake na haivumilii upinzani kwa raia wake."

Rusesabagina aliachiliwa huru mwezi  Machi 25 baada ya zaidi ya siku 939 gerezani, baada ya serikali ya Kigali kubatilisha kifungo chake cha miaka 25 kwa tuhuma za ugaidi.

"Nataka kushukuru serikali ya Marekani kwa kuingilia kati na kushughulikia kesi yangu," alisema.

Kuzuiliwa kwa  Rusesabagina  mwenye umri wa miaka 69, kuliibua suala la kuwa  Rwanda inahusika na  ukandamizaji wa  wapinzani wa kisiasa na uhuru wa kujieleza chini ya utawala wa rais Paul Kagame, ambaye Rusesabagina amekuwa akimtaja kama "dikteta".

Kwa upande wake, serikali ya Rwanda imeendelea kusema haina uhusiano wowote na kinachoendelea katika nchi jirani zake
Kwa upande wake, serikali ya Rwanda imeendelea kusema haina uhusiano wowote na kinachoendelea katika nchi jirani zake REUTERS - JEAN BIZIMANA

Washington imesema Rusesabagina "alizuiliwa kimakosa" baada ya ndege iliyombeba kwenda Burundi kuelekezwa Rwanda mnamo Agosti 2020.

Rusesabagina, anasifiwa kwa kusaidia kuokoa maisha ya takriban 1,200 wakati wa mauaji ya halaiki ya 1994 ambapo takriban watu 800,000 waliuawa, hasa Watutsi lakini pia Wahutu wenye msimamo wa wastani.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.