Wanaharakati wanaendelea kupinga ujenzi wa bomba la kusafirishia mafuta Uganda-Tanzania
Nchini Ufaransa kesi dhidi ya kampuni ya mafuta na gesi TotalEnergies, imeendelea jijini Paris, ambako mashirika sita yasiyo ya kiserikali kutoka nchini Ufaransa na Uganda yamekwenda Mahakamani kupinga kampuni hiyo kuendelea na mradi wa ujenzi wa mafuta kutoka Uganda hadi Tanzania, kwa kile wawakilishi wa mashirika hayo wanasema mradi huo utaharibu mazingira na kukiuka haki za binadamu.
Imechapishwa:
Baada ya kesi hii kuahirishswa mara kadhaa, mawakili kutoka kila upande walishiriki kwenye kesi hiyo iliyoanza mwaka 2019.
Awali kesi hiyo iliahirishwa baada ya mawakili wa wanaharakati hao wanaopinga ujenzi wa bomba hilo kwa kile wanachosema utaharibu mazingira na kuhatarisha maisha ya binadamu, kuomba kuahirishwa kwa kesi hiyo, ili kupata muda wa kujibu utetezi wa kampuni ya Total.
Mwaka 2019, wanaharakati hao kutoka mashirika sita wakiwemo wale nchini Uganda walifika Mahakamani kuishataki kampuni hiyo kwa kukiuka sheria ya Ufaransa ya mwaka 2017 inayotaka ulinzi wa haki za binadamu na mazingira, na kutaka kampuni kusitisha mradi huo.
Licha ya kuendelea kwa kesi hii na wabunge wa Umoja wa Ulaya kupitisha azimio la kupinga mradi huo, rais wa Uganda Yoweri Museveni ameendelea kusisitiza kuwa mradi huu utaendelea kama ilivyopangwa.