WHO inakutana kujadili iwapo Uviko 19 bado ni janga
NAIROBI – Kamati maalum ya Shirika la afya duniani inakutana kujadili iwapo maambukizi ya UVIKO 19 bado ni janga la dunia.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Cheza - 01:06
Huu ni mkutano wa 15 wa watalaam hao, unaokuja miaka mitatu, baada ya kutangaza maambukizi ya ugonjwa huo, ulioripotiwa kutokea nchini China na kuwaaambukiza watu milioni 765 kote duniani, na wengine karibu Milioni saba wakipoteza maisha.
Kamati hii hukutana kila baada ya miezi mitatu kujadili mwenendo wa janga hilo na kutoa ripoti kwa mkurugenzi Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus, ambaye hufanya maamuzi iwapo ugonjwa huo unasalia kuwa janga.
Mkutano huu umefanyika siku nzima, lakini huenda ikachukua siku kadhaa kabla ya matokeo yake kuwekwa wazi.
Mpaka sasa haijawa wazi, watalaam hao watachukua uamuzi gani, lakini kumekuwa na dalili kuwa, huenda WHO ikatangaza kumalizika kwa janga hilo duniani.
Wiki iliyopita, Shirika la afya duniani, lilitanagza kuwa, vifo vinavyosababishwa na maambukizi hayo, vilikuwa vimepungua kwa asilimia 95 tangu kuanza kwa mwaka huu, lakini inaonya kuwa maambukizi hayo bado yapo.
Mkutano huo unakuja pia wakati huu mataifa mengi duniani yakiwa yamelegeza baadhi ya marsharti ya kudhibiti msambao wa Uviko 19 ikiwemo kuondoa ulazima wa uvaaji wa barakoa katika maeneo ya umma.
Aidha mataifa ya Magharibi tayari yameondoa ulazima wa kuwataka wasafiri wa kigeni kuonyesha kuwa hawana maambukizi kabla ya kuingia katika mataifa hayo.