Nchi za kigeni zawahamisha raia Sudan, wakati huu mapigano yakiendelea
NAIROBI – Mataifa ya kigeni yameanza kuwaondoa raia wao nchini Sudan, wakati huu jeshi la taifa na wapiganaji wa RSF wakiendelea kupambana jijini Khartoum, ambapo watu zaidi ya 400 wamepoteza maisha na mamilioni wakikwama ndani ya maakazi yao bila kuwa na chakula na maji.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Raia wa Marekani, Ulaya, Mashariki ya kati na barani Afrika, wanaondoka nchini Sudan kwa kutumia usafiri wa barabara, anga na bahari baada ya kuonekana kuwa vita vinavyoendelea huenda visimalizike hivi karibuni.
Josep Borell, anayehusika na será ya nje ya Umoja wa Ulaya, amethibitisha kuwa tayari raia kadhaa wa mataifa hayo, wameshaondolewa nchini Sudan.
Operesheni yetu imekamilika na imefanikiwa. Kwanza, wafanyakazi wa Umoja wa Ulaya, watu 21 wamefika Ulaya na raia wengine zaidi wa Umoja wa Ulaya, tayari wako nje ya sudan. Siwezi kukupa takwimu kamili, ni zaidi ya watu elfu moja kwa uhakika, Amesema Borell.Mkuu wa sera za Umoja wa Ulaya Josep Borell
Mataifa ya Kenya, Afrika Kusini na Nigeria ni miongoni mwa mataifa ya Afrika, yanayowaondoa raia wake nchini Sudan. Nigeria inasema raia wake karibu Elfu tatu, wengi wao wanafunzi, watapelekwa nchini Misri wiki hii.
Balozi wa Uganda nchini Sudan Rashid Semuddu, amezungumza na Mwandishi wa RFI Kiswahili huko Kampala, Kenneth Lukwago.
Nataka kuwahahakishia kwamba raia wote wa Uganda wako salama, tumewahamisha hadi kwenye mpaka wa Ethiopia, tulikodi mabasi sita kuwahamisha wananchi wetu wote 300, wakiwemo wanadiplomasia, wafanyakazi na wanafunzi. Nafurahi kuripoti kwamba wote hawa wako katika hali nzuri. Amesema SemudduRashid Semuddu, balozi wa Uganda nchini Sudan
Ni vigumu kuelewa vema kinachoendelea kwa sasa nchini Sudan kwa sababu ya kukatika kwa mawasiliano ya simu na Internet, na hata raia wa taifa hilo wameshindwa kuwasiliana vema, huku wengine wakikimbilia katika nji jirani za Misri, Sudan Kusini na Chad.
Hata hivyo, ripoti zinasema kwa kiasi kikubwa siku ya Jumaattu, hali ya utulivu imeshuhudiwa jijini Khartoum wakati raia wa kigeni wakiondoka.
Jeshi na wanagambo wa RSF, wamekuwa wakipigana tangu Aprili 15, kila mmoja akipambana kuchukua madaraka katika taifa hilo la Afrika Kaskazini, huku kila upande ukipuuza wito wa kusitisha vita.