Aliyekuwa kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Benedict wa 16 afariki dunia
Aliyekuwa kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Benedict wa 16, amefariki dunia siku ya Jumamosi, akiwa na umri wa miaka 95.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kifo chake kimejiri siku chache baada ya uongozi wa Kanisa hilo mjini Vatican kutangaza kuwa kiongozi huyo wa zamani alikuwa anaumwa na hali yake afya ilikuwa mbaya.
Taarifa kutoka Vatican zimesema, Papa huyo mstaafu aliyezaliwa nchini Ujerumani, na jina lake halisi ni Joseph Ratzinger, alifariki dunia saa tatu na dakika 34 asubuhi muda wa Vatican, kwa mujibu wa Matteo Bruni msemaji wa Vatican.
Papa Benedict wa 16, aliingia katika vitabu vya historia baada ya mwaka 2013 kujiuzulu, na kuwa kiongozi wa kwanza wa Kanisa Katoliki duniani kuachia nafasi hiyo baada ya miaka 600, kwa kile alichokisema ni kwa sababu umri wake mkubwa na kuanza kudhoofika kwa afya yake.
Aliondoka madarakani, wakati Kanisa hilo lilipokuwa linakabiliwa na kashfa ya makasisi wake kuhusishwa na vitendo vya unyanyasaji wa kimapenzi, vilivyokuwa vimefanyika kwa kipindi kirefu.
Akiwa na umri wa miaka 78, alichagulikuwa kuwa kiongozi wa Kanisa hilo baada ya kifo cha mtangulizi wake Papa John Paul wa pili, baada ya kifo chake mwezi Aprili mwaka 2005.
Baada ya kifo cha kiongozi huyo wa zamani wa Kanisa Katoliki, maombolezo ya siku kadhaa yanatarwajiwa katika mji wa Vatican hadi atakapozikwa.