Djokovic azuiwa nchini Australia akisubiri uamuzi wa Mahakama
Bingwa wa mchezo wa Tennis duniani kwa upande wa wanaume Mserbia Novak Djokovic amezuiwa nchini Australia, baada ya serikali kumfutia tena kibali cha kuwa nchini humo, kushiriki kwenye michezo ya Australian Open inayoanza Januari 17.
Imechapishwa:
Serikali ya Australia ilichukua hatua hiyo baada ya kubainika kuwa, Djokovic hakuwa amepata chanjo na hivyo hana cheti, sharti muhimu la kuingia nchini humo.
Mawakili wake wamekwenda Mahakamani kupinga hatua hiyo ya serikali ya Australia, na sasa mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 34, amezuiwa na idara ya uhamiaji kuelekea kusikilizwa kwa kesi yake siku ya Jumapili.
Hatima ya Djokovic kusalia nchini Australia, kushiriki katika michezo hiyo ambayo amepangwa kucheza siku ya Jumatatu mjini Melbourne, sasa ipo mikononi mwa Mahakama.
Serikali ya Australia imesema ilichukua hatua ya kumfutia kibali Djokovich kwa sababu ya maslahi ya kiafya ya wananchi wake.
Kabla ya kuwasili nchini Australia, jopo la madaktari walimpa kibali Djokovich kushiriki kwenye michezo hiyo bila ya kuchanjwa.
Mwaka uliopita, Djokovic alinukuliwa akisema hana mpango wa kuchanjwa.