Ndege ya Marekani yaua waasi watatu Pakistan
Waasi watatu wameuawa kwa shambulio la ndege ya Marekani isiyo na rubani kaskazini mwa mji wa Wazirstan karibu na mpaka wa Pakistan na Afghanistan, maafisa usalama wamethibitisha.
Imechapishwa:
Eneo lilikofanyika shambulio hilo ni ngome ya kundi la wanamgambo wa Taliban lenye ushirikiano na kundi la Al Qaeda.
Zaidi ya mashambulio 60 ya namna hiyo yameripotiwa kutekelezwa mwaka huu na mashambulizi mengine mengi tangu kuuawa kwa kiongozi wa kundi la kigaidi Al Qaeda,Osama Bin Laden mjini Abottabad nchini Pakistan.
Serikali ya Pakistan imeapa kulinda nchi yake kwa kushirikiana na wadau wengine ikiwemo Marekani ili kuhakikisha kuwa inawasambaratisha waasi ambao wamekuwa tishio kwa usalama wa nchi hiyo.
Hata hivyo uhusiano wa Marekani na Pakistan uliingia doa baada ya kuuawa kwa kiongozi wa kundi la Alqaeda, Osama Bin Laden huku Pakistan ikilaumu Marekani kuingia nchini humo na kufanya shambulizi bila taarifa.
Marekani kwa upande wake ilikuwa ikiituhumu Pakistan kuwa ilifahamu taarifa za kuwepo kwa Osama nchini humo hali ambayo ilikanushwa vikali na serikali ya Pakistan.