Serikali ya Thailand yajipanga kupambana na athari za mafuriko
Waziri mkuu wa Thailand ,Yingluck Shinawatra amewahakikishia wakazi wa mji mkuu wa nchi hiyo Bangkok kuwa serikali inakabiliana na mafuriko ambayo yameuwa watu takribani mia mbili themanini na tisa na kusababisha hasara ya takribani dola bilioni tatu katika nchi hiyo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Yingluck amewaambia waandishi wa habari kuwa mji wa Bangkok unaweza kukumbwa na matatizo kadhaa katika baadhi ya maeneo ambayo yapo karibu na kuta za mabwawa ya umwagiliaji lakini lakini kwango cha maji hakitaongezeka.
Waziri mkuu huyo ameongeza kuwa maeneo ya ndani ya mji huo yana ulinzi wa hali ya juu na kwamba kwa sasa mji huo uchukuliwe kuwa bado ni salama.
Mafuriko yaliyotokea nchini Thailand yamekumba theluthi moja ya eneo la nchi hiyo tangu mwezi Julai huku maeneo ya Kaskazini, Kaskazini Mashariki na katikati mwa nchi hiyo yakiathiriwa vibaya na mafuriko hayo.
Mji wa Bangkok ambao unapatikana mita mbili pekee kutoka usawa wa bahari unaendelea kuwa hatarini kutokana na kuongezeka kwa maji kutoka vyanzo vya maji Kaskazini mwa mji huo ambavyo vinasababisha kufurika kwa mto Chao Phraya.
Baadhi ya wananchi walionekana wakihamisha mali zao na kuzipeleka katika maeneo ambayo hayajaathiriwa.