Xi Jinping kufanya ziara nchini Urusi
NAIROBI – Rais wa China Xi Jinping atazuru Urusi wiki ijayo, wizara ya mambo ya nje ya Beijing imethibitisha siku ya Ijumaa, ikiwa ni safari yake ya kwanza mjini Moscow katika takriban kipindi cha miaka minne.
Imechapishwa:
Xi atazuru jijini Moscow kati ya tarehe 20 hadi 22 mwezi Machi kwa mwaliko wa rais wa Urusi Vladimir Putin.
Kiongozi huyo wa China alifanya ziara ya mwisho nchini Urusi mwaka 2019, ingawa Putin alihudhuria sherehe za ufunguzi wa Michezo ya Olimpiki ya Majira ya baridi huko Beijing mwaka jana na viongozi hao wawili pia walikutana katika mkutano wa usalama wa kikanda huko Uzbekistan mnamo Septemba.
Kwa mujibu wa watu wa karibu na ziara hii, wawili hao watazungumzia masula kadhaa ikiwemo “ushirikiano wa kimkakati.
Ziara hii inakuja wakati huu ikiwa imepita mwaka mmoja tangu Moscow kuivamia Kyiv .
China kwa upande wake imeonekana kuwa nchi isiyoegemea upande wowote katika mzozo huo, lakini msimamo wake umekosolewa na baadhi ya viongozi wa nchi za Magharibi kuwa hawana imani na China kwa kile wanachodai kuwa nchi hiyo inatoa uungaji mkono wa kimyakimya kwa Moscow.
Beijing imekuwa ikitoa wito wa kufanyika kwa mazungumzo kwa pande zote mbili kama njia moja ya kuafikia suluhu ya mzozo unaoendelea kati ya Urusi na Ukraine.
Wizara ya mambo ya nje ya Beijing hakuweka wazi iwapo Xi pia atafanya mazungumzo na rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky.